10 January, 2014

NITOE SIRI ZANGU NA MPENZI WANGU HADI MTAA WA PILI?

Haitoshi kukaa tu pamoja, bali pia ni muhimu kila mmoja AKAJITAHIDI kumuelewa mwenzakejitahidi kumuelewa
Wakati nilipofanya jambo na akaniambia limemkwaa, nilihakikisha kuwa naongea naye kuhusu suala husika na kuhakikisha kuwa tunalipatia ufumbuzi. Sikuwa natumia ubabe kwa kumlazimisha labda kuwa bwana eee…ndio imekuwa hivyo basi sasa unasemaje au kauli zingine kama hizo. Lahasha!! nilitumia lugha ambayo mwishowe iliturejesha katika furaha yetu ya awali.
Tatizo ni kwamba alipofanya yeye jambo lililonikwaza, ninapomuuliza tu, huo ndio ungekuwa mwisho wa furaha yetu kwa siku kadhaa. Hakupenda tujadili kitu pale aliponikosea. Na daima alipenda kuangalia zaidi lugha niliyotumia kuuliza badala ya mantiki ya nilichokuwa nauliza.
Ningeweza kumuuliza “Unadhani mie siumii unapofanya hivyo?” na badala ya kunipa ufafanuzi, akaelewa kuwa hizo ndio hisia zangu na kunipa maelezo ya kunitoa katika hisia hizo mbaya, yeye angekimbilia kusema “Kwahiyo unataka kuniambia kuwa huko nilikokuwa nilikuwa na wanaume sio?” Na hali hii haikuwa mara moja wala mara mbili.
Nilijitahidi sana kuizoea lakini ilinishinda. Ilinishinda maana ilikuwa inaniuliza. Mara nyingi nilijiuliza maswali mengi sana kuliko majibu.
- Je, hanipendi ndio maana anafanya hivyo makusudi na nikiuliza anakwepa kunijibu ili aniumize?
- Je, anathamini sana kazi, shughuli na hata marafiki zake kuliko mimi? Yaani mimi sio kipaumbele chake cha kwanza?
- Ni kwanini hasa ninapoeleza hisia zangu anakuwa mkali badala ya kunijibu kama ninavyomfanyia mimi?
Kwa ujumla mlolongo wa maswali ulikuwa mengi zaidi ya majibu. Sikujua hali hii inatokana na nini. Nilikuwa nafanya kila niwezalo kuhakikisha kuwa simuumizi. Nikimkosea nampa maelezo anielewe ili awe na amani. Nami sikutaka akinifanyia jambo nikwazike milele. Nilipenda sana awe ananipa maelezo ya kutosha badala ya kunifanya niishi kwa vinyongo na kumdhania kuwa hanipendi. lakini haikuwa rahisi namna hii. Ilishindikana.
Nahofia kukaa na kitu kinachonikwaza moyoni maana najua wazi kitanifanya nianze kujenga chuki na yeye. Nitakuwa namshuku vibaya hata kama hanitendei ubaya. Lakini nitafanyaje ilhali hataki pia kunipa nafasi ya kumuuliza? Kila nikimuuliza ananijia juu na tunaishia kugombana? Je, nianze kujadili matatizo ya mpenzi wangu na majirani au watu wengine badala ya yeye? Na je, hao nitakaokuwa nikijadili nao matatizo ya mwenzangu watatupeleka wapi hasa? Si nao watafungua vinywa kuongea na wengine zaidi na mwishowe tutaishia kuanikwa mtaa mzima?



Credit: R. Msangi Via Jukwaa Huru Media Inc.

 

No comments:

Post a Comment

UKIONDOA DIPLOMA, DEGREE AU PHD ULIYONAYO, KICHWA CHAKO KINABAKI NA NINI?

Horace Mann - Binadamu wa kwanza kugundua wazo la elimu Albert Einstein aliwahi kuulizwa akili ni nini? What is intellect? Akasema akili ni ...