10 January, 2014

MNAPENDANA, JE NYOYO ZENU ZINA MAHALI PA KUKUTANIA?

Mapenzi hayatakiwi kuishia tu kutizamana kwa macho. Ni muhimu pia kuhakikisha mioyo ya wahusika inaonana
Hakuna kati yetu ambaye hata sasa anaweza kukataa kuwa hatukupendana. Ndio. Yeye alilijua hilo na hata mimi nililijua hilo. Lakini mwisho wa siku unajua tumeishia wapi? Tumeishia kwa kila mmoja kuchukua njia yake. Yes…tulipendana sana lakini tukaishia kwa kila mmoja kuamua kuangalia upande tofauti na alipo mwenzake. Unataka kujua ni kwanini hasa ilitokea hivi? hebu subiri…….
Wakati Mungu alipoamua kumuumba mwanadamu, kwa makusudi kabisa aliona kuna umuhimu wa kumpa kila mtu kipaji, uwezo, akili na vitu vingine vya namna hiyo kwa namna ya upekee kabisa ambayo ni tofauti kabisa na wengine. Ndio maana duniani kuna msemo wa kuwa “wewe ni mtu maalum, hakuna mwingine kama wewe dunia nzima, hata kama mnafanana majina na maumbo“. Ni kutokana na ukweli huo basi, ambapo binadamu tumekuwa tukitofautiana kimitizamo, kiakili, kimaumbile, nk.
Bahati mbaya sana binadamu tunapofikia umri wa kuingia kwenye mahusiano, ukweli huu tumekuwa tukijitahidi sana kuukwepa. Tumekuwa tunaukwepa ama kwa makusudi kabisa, au kwa bahati mbaya pengine kwa kutokujua. Wengi wetu tumekuwa tukiamini kuwa tunaweza kabisa kuwapata watu wenye kila tunachokihitaji katika maisha yetu. Lakini hebu ona, ni wangapi ambao wameshawahi kuwapata watu wenye kila walichokuwa wakikihitaji?
Ukweli ni kuwa, hata pale ambapo tunawaona watu wakisherehekea Jubilee za miaka kibao ya ndoa zao, haimaanishi kuwa kudumu kwao huko kumetokana na mwanaume au mwanamke husika kuwa alipata kile alichokuwa akikihitaji na ndio maana akadumu nacho.
Ukweli ni kwamba, hata hawa wamepitia milima na mabonde mengi mno. Tena mengi kuliko wale wanaoshindwa mwanzomwanzo wa safari yenyewe ya mahusiano. Na kuthibitisha hili ndio maana kuna msemo wa “Wagombanao ndio wapatanao“….Taarifa za kitaalamu kabisa zinaonyesha kuwa ndoa/mahusiano yale ambayo yamekuwa na migongano ya fikra ya mara kwa mara ndio ambazo zimeweza kudumu kwa muda mrefu.
Muujiza!! Hapana, si muujiza bali ndio uhalisia wenyewe huo. Lakini unajua ni kwanini basi ikawa hivi? Ni kwanini wale wenye kukwaruzana mara kwa mara ndio wenye kudumu zaidi? Lakini kwanini pia wapo wenye kukwaruzana kidogo tu na kila kitu kikawa kimesambaratika? Jibu ni rahisi sana tu…….
Meeting Point.
Wakati fulani nilipokuwa mdogo, nakumbuka tulipokuwa tukicheza mchezo wa kupigana na kila mmoja akawa anamuogopa mwenzake, basi tulikuwa tunachora mstari chini kisha tunasema anayejiamini anatakiwa kuvuka upande wa mwenzake, na hapo ndipo ngumi zingeanza. Wengi wetu tulicheza mchezo huu, hasa wale tuliokulia vijijini. Je, mchezo ule unatufundisha nini tunapokuwa ni wakubwa hivi sasa? Unatufundisha nini kwenye suala la mahusiano?
Mahusiano kama kitu chochote ambacho huwakutanisha watu wawili, ambao kila mmoja ameumbwa tofauti sana na mwenzake, ni kitu kigumu sana. Ni kitu kigumu sana maana ni kitu chenye kumfanya mtu abadilike kwa kila hali.
Mahusiano yaliyo bora kabisa ni yale ambayo hayaendi kwa mtindo wa hisia zangu, au hisia zake, bali hisia zetu. Lakini tunazipataje hisia zetu ilhali kila mmoja ana zake. Je, hisia ni kemikali ambayo unaweza kwenda maabara ukachanganya yako na ya mwenzako mkapata kompaundi moja ambayo inakuwa hisia zenu? Bilashaka jibu ni HAPANA, na kama jibu ni hapana, ni nini basi kinatokea ili kuwa na hisia zenu na sio zako au zake? Subiri nikupe mkasa mmoja:
Siku moja isiyo na jina, nililazimika kukesha kwa kukosa usingizi baada ya kukwaruzana na mtu niliyekuwa nampenda. Ilikuwa baada ya kupishana kauli siku kadhaa kabla ya hapo, ambapo kwenye maongezi yetu niliongea jambo ambalo mwishowe alilitafsiri vibaya. Haikusaidia mimi kujieleza, na baada ya siku kadhaa ndio ikafikia siku hii ambayo aliniambia ni bora asiwasiliane nami kwani nimekuwa nikimuumiza kwa kauli zangu.
Katika usiku huo, nilijiuliza mambo mengi sana, kubwa likiwa ni wapi hasa nilikosea? Cha ajabu sana ni kuwa ndani kabisa ya nafsi yangu, kuna kitu kilikuwa kikiniambia look, hakuna lolote baya ulilolifanya. Ulikuwa na haki kabisa ya kufanya hivyo…tatizo haliko hapo”. sauti hii ilinichanganya sana, lakini mwisho wa siku ilinifanya nizidi kuumiza kichwa zaidi na kwakuwa usiku ulikuwa mrefu sana haikuwa shida baadae kujua tatizo lilikuwa nini.
Chini ya mfumo ule ule wa tofauti za hisia za mwanadamu, nilibaini kuwa licha ya kwamba tulipendana, lakini hatukuwahi kuwa na mahali ambapo hisia zetu zilikuwa zinakutana. Ndio…we never identified the need for a place where our feelings could have been meeting…….
Nilijibaini kuwa kihulka zile zile za hisia za kiuanadamu, mimi nilkuwa ni mtu wa KUSOMA MATENDO YAKE, wakati ambapo yeye alikuwa ameumbwa katika hisia za KUTAFSIRI KAULI ZANGU ZAIDI. Unaona hapo….mmoja msomaji mwingine mfasiri….mmoja maneno…mwingine matendo. Tungeweza kuelewana kweli? Hapana ilikuwa vigumu sana. Ilikuwa ni lazima tupate mahali ambapo hisia zetu zingeweza kukutana. Mahali ambapo fikra zetu zingeweza kukutana. Ilitakiwa tuwe na Meeting Point.
Ndio…hapa ni mahali muhimu sana ambapo tulishindwa kupaandaa…ni mahali ambako tulitakiwa toka mwanzo tuwe tumeshapaandaa kwani hapa ni mahali ambako pangemaanisha kila kitu kuhusu maisha yetu ya mahusiano.
Ni mahali ambapo ningeweza kumwambia Hakuna kwenda disco, na akaelewa kuwa simaanishi akienda anafanya umalaya, bali nina hamu ya kuwa naye ubavuni mwangu kwa muda huo. Hapa ni mahali ambako ningemuuliza kwanini umekawia kurudi nyumbani na akaelewa kuwa nilitamani sana nikute yuko nyumbani anipokee na sio kuwa nilimaanisha kuwa amepitia mahali pabaya. Ndio…hapa ni mahali ambako angeniambia nataka kwenda kwa rafiki yangu nami nikaelewa kuwa anaona nimechoka anataka nipumzike kwa utulivi kwakuwa akiwepo hawezi kuvumilia kunisemesha……Kifupi, hapa ni mahali ambako pangekuwa kila kitu.
Ni katika usiku huo huo nilipowaza na kujua kuwa kumbe tulifanya makosa makubwa sana kutokukubaliana katika hili. Tulikosea sana kuamini kuwa ningeweza kumpenda naye akaonyesha kunipenda wakati hatupendani. Ni usiku huo nilipobaini kuwa kumbe tulichokuwa tukifanya ni sawa na mimi kuuvuta moyo wake, huku yeye naye akiuvuta wangu..kumbe tulitakiwa tusivute moyo wa kila mmoja bali tuunganishe nyoyo zetu. Lakini tungefanyaje ilhali hatukuwa na meeting point? Sikuwa napita katikati ya mistari ya kile alichokuwa akitenda. Hakuwa akipita katikati ya mistari ya kile nilichokuwa nikikisema………….Hatukuwa na mahali tulipokuwa tunakutanisha hisia zetu…huyu akajua ni kwanini yule alifanya vile na kwanini huyu akasema hivi……..

No comments:

Post a Comment

UKIONDOA DIPLOMA, DEGREE AU PHD ULIYONAYO, KICHWA CHAKO KINABAKI NA NINI?

Horace Mann - Binadamu wa kwanza kugundua wazo la elimu Albert Einstein aliwahi kuulizwa akili ni nini? What is intellect? Akasema akili ni ...