27 September, 2013

RAIS KIKWETE: NITAAMRISHA JESHI KUPAMBANA NA MAJANGILI

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete ametangaza kuwa ataliamrisha Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) kuongoza mapambano dhidi ya ujangili wa tembo na faru na ukataji haramu wa miti kwa shughuli za biashara ambao umefikia kiwango kikubwa Tanzania.
Aidha, Rais Kikwete amesema kwamba sekta ya utalii katika Tanzania sasa imeanza kutishiwa kweli kweli na uuaji wa wanyama hao na biashara haramu ya meno ya tembo na faru na kuwa tishio hilo ni kubwa kwa sababu sekta ya utalii inachangia kiasi cha asilimia 17 katika Mapato ya Taifa na inaajiri kiasi cha watu 300,000.
Rais Kikwete ametangaza uamuzi huo makini jioni ya leo, Alhamisi, Septemba 26, 2013 wakati alipozungumza kwenye Mkutano wa Viongozi wa Nchi na Serikali kuhusu biashara haramu ya wanyama na bidhaa zake pamoja na biashara haramu ya bidhaa za miti na mbao.
Rais Kikwete ameuambia Mkutano huo ulioandaliwa na Rais Ali Omar Bongo Ondimba wa Gabon na Serikali ya Ujerumani kwenye Makao Makao ya Umoja wa Mataifa kuwa mwaka 1960, Tanzania ilikuwa na tembo kiasi cha 350,000 lakini kutokana na ujangili idadi hiyo ya tembo ilishuka hadi 110,000 ilipofika mwaka 2009. Kuhusu faru, Rais Kikwete amesema kuwa mwaka 1974 walikuwepo faru 700 katika Tanzania na sasa wako chini ya 100 kwa sababu ya vitendo vya kijangili.
“Katika miaka ya 1980 na 1990 wakati wa kilele cha ujangili katika mikonga ya wanyama, tulilazimika kutumia jeshi kutuliza hali hiyo. Tuliona matokea mazuri na tulikuwa na utulivu wa aina fulani. Lakini katika miaka minne iliyopita, tumeshuhudia kuongezeka kwa vitendo vya ujangili kwa ari na kasi mpya. Kwa mfano kati ya mwaka 2010 na Julai, mwaka, 2013, zaidi ya tembo 1,386 waliuawa katika Tanzania.”
Ameongeza Rais Kikwete: “Tumechukua hatua kali za kupambana na ujangili ikiwa ni pamoja na sera, sheria na kanuni za kupambana na ujangili. Aidha, tumetia saini mikataba mbali mbali ya kimataifa ya kupambana na ujangili huu.” Amesema Rais Kikwete na kuongeza:
“Vile vile, tumechukua hatua za kukamata majangili na hata kukamata silaha zinazotumika katika ujangili. Kati ya mwaka 2010 hadi katikati ya mwaka huu, 2013, jumla ya majangili 5,189 wametiwa mbaroni na silaha kiasi cha 1,952 zimekamatwa. Isitoshe, vipande vya 3,788 vya meno ya tembo vimekamatwa vikiwa na uzito wa kilo 10,756 zilikamatwa nchini. Nimeamuru Jeshi la Wananchi wa Tanzania kukabiliana na hali hiyo na naamini kuwa tutapata mafanikio makubwa zaidi katika operesheni inayoandaliwa.”
Hata hivyo, Rais Kikwete amesema kuwa bado shughuli za kupambana na ujangili, zinakabiliwa na changamoto nyingi ikiwa ni pamoja na mahitaji ya watumishi 4,800 wapya kwa ajili ya kupambana na ujangili hata kama wameajiriwa wafanyakazi 500 tu mwaka huu.
“Pamoja na kwamba tuna matatizo ya watumishi, bado pia tuna matatizo ya raslimali fedha. Bajeti ya sasa ya dola za Marekani 6.9 milioni kwa ajili ya Idara ya Wanyamapori haitoshi kutimiza yote haya. Tunahitaji dola za Marekani milioni 19.4 kwa ajili ya shughuli hiyo na nyongeza ya dola milioni 30 kwa ajili ya ununuzi wa vifaa na ujenzi wa nyumba za wafanyakazi. Tukiachiwa pekee yetu hatuna uwezo. Tunaomba twende pamoja katika hili.”

Chanzo:Kibonde

No comments:

Post a Comment

UKIONDOA DIPLOMA, DEGREE AU PHD ULIYONAYO, KICHWA CHAKO KINABAKI NA NINI?

Horace Mann - Binadamu wa kwanza kugundua wazo la elimu Albert Einstein aliwahi kuulizwa akili ni nini? What is intellect? Akasema akili ni ...