05 August, 2014

TUME YA WARIOBA YAIVUA NGUO SERIKALI, YASEMA WANAPOTOSHA KUHUSU KATIBA MPYA

Aliyekuwa Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji mstaafu Joseph Sinde Warioba

JANA taifa lilisimama saa nne kwa Watanzania kuelekeza masikio na macho kwenye runinga kusikiliza ufafanuzi wa wajumbe wa iliyokuwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, juu ya upotoshaji wa viongozi waandamizi wa serikali kuhusu mapendekezo yaliyomo kwenye rasimu ya katiba mpya.
Wajumbe wa Tume hiyo wakiongozwa na Jaji mstaafu Joseph Warioba, waliwataja viongozi hao kuwa ni Stephen Wassira, William Lukuvi, Anna Tibaijuka na Mwigulu Nchemba katika mdahalo wa katiba mpya uliofanyika Ukumbi wa Ubungo Plaza jijini Dar es Salaam, uliondaliwa na Taasisi ya Mwalimu Nyerere na kurushwa na runinga ya ITV.
Jaji Warioba, alianza kwa kuweka hadharani namna watu wenye propaganda za mfumo wa serikali mbili wanavyopotosha maana nzima ya rasimu ya pili ya tume hiyo inayoelekeza mfumo wa serikali tatu.
Alisema watetezi wa serikali mbili, wamejikita kuelezea upungufu wa serikali tatu huku wakiacha mazuri ya muundo huo pamoja na udhaifu wa serikali mbili za sasa.
Jaji Warioba, alikanusha kauli iliyotolewa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera na Bunge, William Lukuvi, kuwa kuna maoni mapya yamewasilishwa serikalini.
Alisema hajabadilika katika msimamo wake wa kutetea serikali tatu kama wananchi walivyotaka, na kwamba kinachofanywa na wanaoeneza maneno hayo ni uzushi wenye malengo maalum.
Alifafanua kuwa kilichofanywa na wao ni kupeleka serikalini yale mambo ambayo waliyachuja na ambayo yasingekuwa na nafasi katika Serikali ya Muungano zaidi ya kusubiri Katiba ya Tanganyika.
“Sijabadilika, na jambo la msingi ni kwamba yale tuliyoyachuja badala ya kutupa tulisema tukakabidhi serikalini kwa ajili ya kusaidia kuwa kumbukumbu kwao pale watakapoona wanakwama, lakini muhimu hayo wanayosema tumepeleka kuonyesha kuwa tumebadilika ni vema waweke hadharani,” alisema Jaji Warioba.
Alisema bado kuna haja ya viongozi kuendelea kuvumiliana na kutafuta maridhiano yatakayozaa katiba bora ya Watanzania, huku akibainisha kuwa hata wao walikuwa na tofauti zilizomalizwa kwa kuangalia maslahi ya taifa badala ya makundi waliyotoka.
Kwamba kabla ya Bunge la Katiba kuanza, aliwashauri viongozi wa vyama vya siasa kukutana na kukubaliana baadhi ya mambo, na kwamba viongozi hao hawakuweza kufanya jambo hilo, hali iliyozalisha matokeo ya sasa ya mchakato ulipofikia.
Jaji Warioba alikataa dhana ya wanasiasa na wachambuzi mbalimbali wanaotaka Bunge hilo liahirishwe kwa muda kuchagua baadhi ya mambo yatakayofanyiwa maboresho huku yakitajwa kuwa ni kuboresha Tume ya Uchaguzi na kutoa fursa kwa mgombea binafsi.
Alisema, haafiki mambo hayo kuwa kipaumbele na kuachwa kwa mambo muhimu ya wananchi.
Aliyataja baadhi ya mambo muhimu ya kujadiliwa mbali na masuala ya uchaguzi, kuwa ni pamoja na suala la uwazi na uwajibikaji, kwa madai kwamba huwezi kuwa na utawala bora kama hakuna uwazi na uwajibikaji.
Pia, alisema suala la maadili na tunu ya taifa ni mambo ambayo wananchi walizungumzia sana na haki za binadamu ambako walitaka kuwekwa kwa utaratibu wa utekelezaji kwa kuwa hata zilizopo hazitekelezeki.
Aidha, Jaji Warioba aliwashangaa wale wanaohangaika na takwimu, lakini akasisitiza kuwa itambulike wajumbe wa tume ndio waliozunguka mikoani na kuzungumza na wananchi na kuna mengi yalisemwa kwa uwazi kabisa ambayo wengi hawayajui.
Paramagamba aonya
Kwa upande wake, Profesa Paramagamba Kabudi akichangia katika mjadala huo, aliasa kuzingatia utu na kuheshimu mawazo ya wengine.
Alisema kwa upande wake, hawahofii Wazanzibar kwa kuwa wao wanayo mambo yao na yanayojulikana, na kwamba Watanganyika mambo yao wameyaficha mioyoni, jambo aliloeleza kuwa ni hatari kama hawatapatiwa mahitaji yao mapema.
Alisema kwamba ni wakati muafaka hivi sasa Watanganyika wakapewa serikali yao wakiwa wanaidai kwa amani, badala ya kusubiri waongezeke na kuidai kwa nguvu.
“Ni busara kuwapa Watanganyika serikali yao wakati wanaiogopa, badala ya kusubiri waidai wakati wakiwa wengi na muda wa kuwaongoza ukiwa haupo,” alisema Profesa Kabudi na kutoa mfano wa Baba wa Taifa, Mwalimu Nyerere, ambaye wakati wa mchakato wa taifa kuingia mfumo wa vyama vingi miaka ya 90 mwanzoni, licha wakati ule waliokuwa wakitaka vyama vingi walikuwa wachache, alivikubali, kwani alijua ni bora kuliko waliokuwa wakiunga mkono wangepuuzwa na kuja kuvidai kwa nguvu.
Kuhusu muundo wa rasimu, Profesa Kabudi alisema inatoa fursa ya rais wa muungano kushitakiwa kwa uhaini kama atakiuka mambo yaliyoamuliwa na mahakama ya muungano.
Alisema tatizo kubwa lililopo, ni kwa watu waliojivika upumbavu kushupalia kila jambo hata kama hawana uwezo nalo, wakiamini nguvu zitawalinda huku akisisitiza kuwa, hakuna aliye mkubwa juu ya sheria.
Butiku amshangaa rais
Mwenyekiti wa Taasisi ya Mwalimu Nyerere, Joseph Butiku, kwa upande wake alieleza kuwa Rais Kikwete alipokubali mchakato wa katiba na kuunda tume, hakuwa na mamlaka ya kuiingilia tena.
Alisema jambo la msingi ni wahusika kufuata kile kilichokusanywa kwa wananchi na kuheshimu, badala ya yale wanayoyakwaza kwenda kupata ushauri ndani ya chama.
“Ninyi simamieni kile mnachoamini kilichokusanywa na tume, hapa hakuna nani wala nani, hata Wassira hayupo, watu wanasema tume imesema uongo, lakini tunajua namna umri wetu ulivyo, tutasema uongo kwa ajili ya nini, huu mchakato ni wa wananchi,” alisema Butiku.
Alisema katika mazingira ya sasa wanapoamua kusema wanaitwa wachochezi, na kwamba wananchi wanapaswa watafakari kwanini baadhi ya vitabu walivyokusanyia maoni vimefichwa na tovuti ya tume imefungwa.
Aliongeza kuwa Jaji Warioba anaficha baadhi ya mambo, ikiwamo kueleza wazi kuwa kutungwa kwa katiba ya Zanzibar ya 2010 kulivunja uwepo wa muungano.
Alipoulizwa kama hotuba ya Rais Kikwete aliyoitoa bungeni iliharibu mchakato mzima wa Katiba Butiku, alisema nchi ina Rais na anaheshimiwa sana na kwamba heshima ina pande mbili huku akizitaja kuwa njia mojawapo ya kumheshimu rais ni kutokuficha ukweli na kwamba upande wa pili ni heshima ya kuficha ukweli.
Alisema mtu atakayeficha ukweli atakuwa hamuheshimu rais, na kwamba kitendo cha kusema hakushauriana na tume kinapaswa kifikiriwe kwa makini kwa kuwa wao walishauriana nae vya kutosha.
Butiku alisema rais anapaswa kuheshimiwa na hata eneo alilotolea kauli hiyo linapaswa kuheshimiwa, na kwamba muhimu Watanzania wajue kuwa walishauriana kwa kina.
Polepole afichua siri
Aliyekuwa mjumbe wa tume hiyo, Humphery Polepole, alisema wakati wakikusanya maoni, viongozi mbalimbali wa kiserikali waliojitokeza mbele yao walitaka muundo wa serikali tatu na hata tasisi wanazozisimamia zilibainisha umuhimu wake.
Alizitaja taasisi hizo kuwa ni Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano, Tume ya Makatibu na Viongozi wa Serikali ya Zanzibar, pamoja na Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa.
Alisema anapowaona baadhi ya viongozi waliotoa maoni ya serikali tatu wanavyotumia nguvu ya kutaka serikali mbili wakiwa hadharani, anashindwa kuwaelewa wana dhamira gani kwa Watanzania.
Kuhusu gharama za Serikali ya Muungano, Polepole alisema hakuna gharama kubwa zaidi ya kupunguza matumizi na kubainisha kuwa haziwezi kuzidi sh trilioni 2.
Awadh Said ashangaa madai ya gharama
Mwanasheria Awadh Said ambaye naye alikuwa mjumbe wa tume hiyo, alisema anashangazwa na watu wanaokimbilia takwimu na gharama katika suala zima la rasimu huku wakishindwa kuainisha idadi ya wabunge watakaopungua kwa kupatikana serikali tatu.
Alisema muundo mzima wa wabunge wote wa muungano kwa sasa una watu 434 na kwamba katika Serikali ya Muungano iliyopendekezwa idadi hiyo itapungua kwa wabunge 100.
Kwamba tume haikuelekezwa ichukue takwimu bali uzito wa hoja, na kwamba hoja zilizotolewa ndizo zimezaa rasimu iliyopo.
“Nashangaa wengine wanajiita wachumi huku wakishindwa kuona namna gharama zitakavyopungua katika muundo wa serikali tatu, lakini katika hali ya sasa wanapaswa watuambie ni wizara gani inayofanya kazi yake Zanzibar ukiacha zile za muungano na sana sana ile ya Mambo ya Ndani,” alisema huku akihoji kama Wizira ya Nyumba na Maendeleo ya Makazi imewahi kwenda kusimamia maendeleo ya ardhi Zanzibar.
Aliongeza kuwa kwa sasa Zanzibar inajisimamia kwa masuala mbalimbali, ikiwamo ardhi, hivyo kusema uwepo wa serikali tatu ni gharama ni kuudanganya umma.
Awadh alisema suala la muungano kwa bahati mbaya linazungumziwa na watu wasiolielewa au hawapendi kufuatilia mambo, zaidi ya kutengeneza propaganda na vitisho.
CREDIT: TANZANIADAIMA: TUME YA WARIOBA YAIVUA NGUO SERIKALI

No comments:

Post a Comment

UKIONDOA DIPLOMA, DEGREE AU PHD ULIYONAYO, KICHWA CHAKO KINABAKI NA NINI?

Horace Mann - Binadamu wa kwanza kugundua wazo la elimu Albert Einstein aliwahi kuulizwa akili ni nini? What is intellect? Akasema akili ni ...